TSH BIL 20.21 ZATENGWA KWA AJILI YA WENYE ULEMAVU
TANZANIA
Serikali imetenga shilingi bilioni 20.21 katika mwaka wa fedha 2024/2025 kwa ajili ya watu wenye ulemavu (PWDs) kutoka shilingi bilioni 16.14 ya mwaka 2023/24 ambazo ni mikopo isiyo na riba kutoka asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri.
Aidha kupitia Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Huduma za Miradi (UNOPS), serikali imepata ruzuku ya shilingi bilioni 8.2 kwa ajili ya kutekeleza mradi wa uchunguzi wa watoto wenye ulemavu wa kuona na kusikia ambapo wale ambao watatambuliwa kuhitaji vifaa vya msaada watapokea bila malipo.
Mradi huu utaanza Novemba 2024, ukiwanufaisha zaidi ya watoto 300,000 wenye changamoto husika.
Pamoja na hayo katika mwaka wa fedha 2024/2025, Serikali ina mpango wa kujenga miundombinu ya elimu inayofikika kwa urahisi, ikiwa ni pamoja na vyumba vya madarasa 6,357, vyoo 1,482, kumbi 362 za kulia chakula na mabweni 36.
