TSH MIL 528 ZAWAOKOA WATOTO KUTEMBEA KM 21

 

TSH MIL 528  ZAWAOKOA WATOTO KUTEMBEA KM 21

TSH MIL 528  ZAWAOKOA WATOTO KUTEMBEA KM 21

MOROGORO
Wananchi wa Kijiji cha Ruhembe, Halmashauri ya Wilaya ya  Kilosa Mkoani Morogoro wameonesha furaha yao baada ya serikali kutoa kiasi cha shilingi milioni 528  kwa ajili ya kujenga shule mpya ya sekondari Miwa kupitia mradi wa Kuboresha Elimu ya Sekondari (SEQUIP).
Mwenyekiti wa Kijiji cha Ruhembe Abdallah Kambi  amesema "Kiukweli kwa sasa wananchi hatuna adha tena ya shule ya sekondari katika hiki kijiji tunamshukuru sana  Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kupambana kuwekeza miradi ya elimu."
Ameongeza kwamba hapo awali watoto wa kijiji hicho walikuwa wanapata changamoto ya kwenda shule umbali wa kilomita 21 sababu ikiwa ni  umbali na makazi na jiografia ya kijiji hicho kimezungukwa na mashamba ya miwa maeneo mengi yanaonekana  ni pori,ambapo watoto walikuwa wanakumbana na matukio  mengi na hasa kwa watoto wa kike kufanyiwa vitendo vya kikatili.
Ameongezea kwa kusema watoto hao ( hasa wa kike) walikuwa   wanashindwa kumaliza shule  sababu ya changamoto zikiwemo za umbali wa shule waliokuwa wanaenda, kufanyiwa vitendo visivyofaa kama kubakwa, kupata ujauzito na mambo mengine ambayo yalikuwa ni changamoto kwa watoto hao wakike.
Naye mkazi wa Kijiji hicho Fitina Nganywela amesema uwepo wa shule hiyo imewasaidia pia  wao kama wazazi kuwa na imani na watoto wao sababu shule hiyo ipo karibu na maeneo ya makazi ambapo ni rahisi hata kwa mzazi kumfuatilia mtoto maendeleo yake shuleni na mwenendo mzima wa elimu.