DARAJA LA MZINGA , BARABARA YA MBAGALA KUJENGWA
DAR ES SALAAM
Serikali inafanya maandalizi ya ujenzi wa miradi mikubwa inayolenga kupunguza msongamano wa magari katika eneo la daraja la Mzinga Mbagala wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam.
Miradi hiyo ni upanuzi wa barabara kutoka Mbagala Rangi Tatu hadi Kongowe yenye urefu wa Kilometa 3.8 kwa kiwango cha lami na ujenzi wa daraja jipya la Mzinga ambayo itatumia kiasi cha shilingi 177,296,700,000 ufadhili kutoka Benki ya Dunia kupitia Mpango wa Dharura (Crisis Response Window).
Manunuzi ya miradi hii yanatarajiwa kukamilika Januari 31, 2025, na mkandarasi atapatikana Februari 2025 na Ujenzi wa barabara na daraja vitaanza mara moja
Daraja la sasa la Mzinga lenye urefu wa mita 45 na upana wa mita 9 litaongezewa njia mbili kila upande na sehemu ya mabasi yaendayo haraka, huku barabara ya Mbagala Rangi Tatu hadi Kongowe ikipanuliwa kuwa na njia sita pamoja na maeneo ya watembea kwa miguu na waendesha pikipiki.
Aidha Ujenzi wa miradi hii ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutatua changamoto za msongamano jijini Dar es Salaam.